Saturday, November 17, 2012

UPENDO


1 Yohana 4:16"Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake".
Upendo wa Mungu wetu ni mkuu sana na unapita vitu vingi mno. Hata mtu akianza kuandika leo hii juu ya Upendo wa Mungu wino utakwisha kwa maana ni mkubwa mno hauelezeki. Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa mwana wake wa pekee Yesu Kristo ili kila amwaminie yeye asipotee bali awe na uzima wa milele. Yesu alitufia msalabani kwa ajili ya dhambi zetu, hii inadhihirisha jinsi gani Mungu amempenda mwanae huyo wa pekee afe kwa ajili ya mimi na wewe.
Upendo huleta amani, furaha na faraja. Ndani ya moyo wangu nina amani tele na furaha. Nampenda Kristo kwa sababu ameniokoa kwa damu ya thamani. “Utanijulisha njia ya uzima; mbele za uso wako ziko furaha tele; na katika mkono wako wa kuume mna mema ya milele,” Zaburi 16:11
Upendo hutoka kwa Mungu na kila mwenye upendo ni mtoto wa Mungu. “Twampenda yeye kwa sababu yeye alitupenda kwanza na akaichukua mioyo yetu kwake mwenyewe” 1 Yohana 4:19. Hakuna kitu muhimu katika maisha ya binadamu kama UPENDO.Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabiri; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote. Upendo haupungui neno wakati wowote - 1Wakorintho 13:4-8
Mtu mwenye kukosa upendo huyo hayuko ndani ya Kristo na siku zote huwa na chuki. Hata katika Biblia imeonyeshwa kwamba mtu akisema anampenda Mungu ana anachukia ndugu yake ni muongo. “1Yohana 4:20 Mtu akisema, nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona”.
Si vyema kuchukiana juu ya mambo madogo madogo.Huna sababu ya kumchukia ndugu yako sababu ya wivu ama kumchukia jirani yako sababu ana maendeleo ambayo wewe huna. Hata amri ya pili inasema mpende jirani yako kama nafsi yako, sasa iweje unamchukia jirani ama ndugu yako wa kuzaliwa naye. Hii haimpendezi Mungu na yakupasa kumrudia yeye na kujifunza neno lake ndipo utaelewa maana halisi ya upendo.  Tuzishike amri za Mungu na kukaa katika pendo lake.
Upendo haujalishi umpendaye ni tajiri ama maskini. Kuna watu ambao huchagua watu wa kuwapenda yaani ambao wanaona wako kwenye status zao. Huo sio upendo bali ni kutafuta watu ambao unadhani utapata furaha kwa sababu tu pengine anaendesha benzi, anakula sehemu za bei ya juu, anavaa vitu vya bei na vitu vingine vinavyofanana na hivyo.
Tuwe na upendo wapendwa kwa sababu ukiwa na upendo siku zote utakua na amani. Kwa maana mtu mwneye Upendo hulipa mabaya kwa mazuri, kamwe hawi wenye visasi. Mwenye upendo siku zote ni mnyenyekevu mbele za watu na hujali wengine zaidi yake mwenyewe.
Usiruhusu mwanadamu akurudishe nyuma na ukatoka katika pendo. Binafsi tangu niijue Biblia maisha yangu yamekuwa ya furaha sana na amani. Na ndiyo maana nasema maisha yangu ni biblia yangu mahali ambapo napata faraja kila nisomapo. Through biblia nimejifunza nini maana halisi ya upendo, na mambo mengine mazuri.
Tujitunze katika upendo wa Mungu, huku tukingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele. Na haya yote yanapatikana kwa kumuomba roho mtakatifu akuongoze uwe na upendo.
Mimi nawapenda, muwe na Jumapili njema.

Thursday, November 15, 2012

Ujumbe wa leo


"Msitende neno lolote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine. Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu" Wafilipi 2:3-5
Mungu anakupenda ndiyo maana unaishi mpaka leo hii. Mungu wetu hapendezwi na majivuno wala kiburi hupendezwa na wale wenye unyenyekevu. Mungu anatuasa kuacha majivuno na kujiona ni bora kuliko mtu mwingine. Pia anasema tuache kushindana kwa lolote hususan yale tunayoshindania hayana baraka kwake wala hayajengi. Ubinafsi usichukue nafasi ndani ya mioyo yetu, hii itasababisha kututenga mbali na Mungu kwa maana mtu binafsi na mwenye kufanana na mambo kama hayo huhesabiwa maovu na baba yetu wa mbinguni.
Mbarikiwe!

Wednesday, November 14, 2012

Zaburi ya Leo

Zaburi 119: 41-48 "Ee Bwana, fadhili zako zinifikie na mimi, naam wokovu wako sawasawa na ahadi yako. Nami nitamjibu neno anilaumuye, kwa maana nalitumainia neno lako. Usiliondoe neno la kweli kinywani mwangu kamwe, maana nimezingojea hukumu zako. Nami nitaitii sheria yako daima, naam milele na milele. Nami nitakwenda panapo nafasi, kwa kuwa nimejifunza mausia yako. Nitazinena shuhuda zako mbele ya wafalme, wala sitaona aibu. Nami nitajifurahisha sana kwa maagizo yako ambayo nimeyapenda. Na mikono yangu nitayainulia maagizo yako niliyoyapenda, nami nitazitafakari amri zako".
Muombe Mungu akupe fadhili zake na udumu katika neno lake. Kwa maana ni neno lake pekee litatuokoa. Songa mbele usisikilize watu wasemayo na siku zote mwanadamu hakosi la kusema. Iwe ni juu ya mafanikio yako ama jambo lolote bado kutakuwa na neno juu yake. Mtumainie Mungu na umuombe sana asiliondoe neno lake kinywani mwako. Zitafakari na kuzifuata amri zake hakika utaona uzuri wa kuishi kwa kumtegemea Mungu.

Mbarikiwe sana!

Sunday, November 11, 2012

Mstari wa Leo


"Kiburi cha mtu kitamshusha, bali mwenye roho ya unyenyekevu ataheshimiwa" Mithali 29:23
Mbali na haya maneno ya Biblia juu ya kiburi pia katika maisha ya kawaida kuna methali inasema "kiburi si maungwana". Mtu mwenye kiburi hukosa mengi kwa watu na hata hujikosesha baraka zake toka kwa Mungu. Na ndiyo maana anasema kiburi cha mtu kitamshusha lakini yule mwenye kunyeyekea atapata heshima pamoja na kupata mema.
Unaposoma neno hili kaa utafakari na kama wewe ni mwenye kiburi, jiulize umepata mangapi kutokana na kiburi chako, umekosa mangapi na kimekufikisha wapi? Kumbuka moyo wenye kiburi humchukiza Bwana.
Kiburi hakijifichi, na pengine mwenye kiburi anaweza asione anacho lakini watu wengine wanaweza kutambua kwa haraka kiburi kilichopo ndani ya mtu.
Muombe Mungu akusaidie akuondolee kiburi na akupe moyo wa unyenyekevu upate yaliyo mema. Mara nyingine tunashangaa kwa nini hatuendelei kifedha, kiafya na hata katika mahusiano huoni kilicho cha manufaa, lakini huwezi jua pengine ni kiburi chako hukwamisha hayo yote.

Muwe na wiki yenye kuzaa matunda katika kazi zenu!

FUNGU LA KUMI/ THITHE


Fungu la kumi ni ile asilimia kumi ya mazao ama kipato cha mtu anachopata ambacho anatenga kwa ajili ya kumtolea Mungu.
Kwa kiingereza THITHE is the tenth part of agricultural produce or personal income set apart as an offering to God or for works of mercy, or the same amount regarded as an obligation or tax for the support of the church, priesthood, or the like. OR is a tenth part or any indefinitely small part of anything.
Asilimia 10 ya kipato chako unachotakiwa umtolee Mungu kinatakiwa kiwe kwenye gross salary na sio net salary. Katika hili wapo wenye mtazamo tofauti ya kwamba 10% inatoka kwenye net salary yaani baada ya makato. Binafsi mimi 10% yangu nahesabia kipato changu chote kabla ya makato. Natoa kwa moyo nikijua ya kuwa Mungu pekee ndo atanizidishia. Kumbuka ukitoa extra Mungu nae huona moyo wako ulivyo mkunjufu.
Watu wengi wanapatwa na vishawishi vya kuuliza pindi watoapo fungu lao la kumi ama sadaka zao kuwa zinaenda wapi. Epuka kishawishi cha namna hiyo kwa sababu kinakuzuia kupata baraka za Bwana. Kama utawala wa Kanisa utatumia fungu hilo la kumi kwa kufanya mambo yamchukizayo Mungu, ni juu ya yeye kuwahukumu. Mungu anakujua ya kwamba umemtolea na yeye atakubariki kwa sababu amependezwa na wewe. Kwa kujenga huu msingi wa utoaji fungu la kumi Mungu atakubariki kwenye masuala ya utajiri ambao ni mali, fedha, afya, usalama wako na mambo mengine yanayofanana na hayo. Kwa kifupi utauona mkono wa baraka wa Bwana katika nyanja mbali mbali za maisha yako. Mfano mzuri katika Biblia Kitabu cha Mwanzo 22 ni pale Ibrahimu alipomsikiliza Mungu pale alipotaka amtoe sadaka mwanae wa pekee Isaka. Alipotaka kufanya hivyo akasikia sauti ya Mungu ikimuasa asimtemdee mwanae hivyo kwa maana sasa amejua ya kuwa anamcha Mungu. Ule mstari wa 17 unasema “ katika kubariki nitakubariki na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni na kama mchanga ulioko pwani na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao”
Jenga tabia ya kutoa kwa kuwa utoaji wako unampa Mungu heshima na utukufu. Ni sehemu kubwa ya utukufu. Mtolee Mungu kwa moyo wako wote na sio kutoka kana kwamba unamkopesha Mungu. 2Wakorintho 9:7 “Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala kwa lazima maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu”
Agano la kale linaonyesha kwamba watu walikuwa wakitoa mazao,na wanyama walionona kama fungu la kumi. Kwa ulimwengu wetu wa sasa ambapo watu wengi tumeajiriwa, fungu letu la kumi litahesabiwa kwenye kipato tupatacho katika kazi zetu ama biashara tufanyazo.
Katika kitabu cha Mithali 3:9 “Mheshimu BWANA kwa mali zako na kwa malimbuko ya mazao yako yote, ndipo ghala zako zitakapojaa hadi kufurika, viriba vyako vitafurika kwa mvinyo mpya.”
Pesa kwa sasa imekuwa ngumu na ndiyo maana watu wengine wana mitazamo tofauti ya fungu la kumi. Mtu mwingine anakuambia siwezi toa fungu la kumi kwa sababu sioni likizungumziwa kwenye Agano jipya. Lakini hii ni kutokana na ugumu wa utoaji na upofu wa mtu wa kujua ya kuwa ukimtolea Mungu kazi zako za mikono zinabarikiwa mara dufu. Na pili watu wamekuwa wakiiabudu sana pesa na kusahau kuwa Mungu huyo huyo ndo ametupa uweza wa kutawala vitu kama hivyo.
WAPI NATOA FUNGU LA KUMI
Malaki 3:10 “Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo asema Bwana wa majeshi, mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha au la”
Toa fungu lako la kumi nyumbani kwa Bwana ambapo ni mahali unapokwenda kumwabudu yaani Kanisani. Kama umepanga kutoa fungu la kumi litoe hiyo siku uliyopanga, kwa kufanya kinyume chake utakuwa unamuibia Mungu. Kumuibia Mungu maana yake umepanga kutoa fungu lako la kumi kesho halafu inapofika siku ya kutoa unabadili mawazo ama kutoa fungu pungufu, hivyo ni kumuibia Mungu. Mtolee Mungu kwa wakati ulioahidi bila kukoma.
Ninavyoelewa kusaidia wajane, yatima, na wasiojiweza hiyo haihesabiwi kama fungu la kumi, bali inaingia katika upandaji mbegu, yaani kusaidia watu kwa moyo bila kusubiria mrejesho.Nasema hivyo kwa sababu wapo watu wanatoa msaada kwa yatima ama mtu asiyejiweza na kusema hili ndilo fungu langu la kumi. Mmoja wapo ni mimi nilikuwa nasema Mungu niongoze na nifunulie hii pesa nimpe nani ambaye anahitaji zaidi nikijua kuwa ni sehemu yangu ya fungu la kumi bila kujua nilikuwa namuibia Mungu. Kwa hiyo mtu aliyekuwa ananijia kichwani ndiyo nilikuwa nampelekea na kusema kwamba nimetoa fungu la kumi.

KUPANDA MBEGU
Pamoja na kutoa Fungu la kumi, ni vizuri kujenga tabia ya kupanda mbegu yaani kutoa fedha, msaada kwa watu mathalan yatima, wajane na wenye shida mbali mbali kwa nia ya kuvuna mema kutoka kwa Mungu. Kwa kifupi jenga tabia ya kusaidia watu lakini isiwe unafanya mfano kwamba unawekeana mkataba na Mungu ya kuwa ninamsaidia mtu fulani basi lazima Mungu aniongezee. Kwa kufanya hivyo hutafanikiwa kwa sababu unakuwa hujatoa kwa moyo wako wote. Mfano mzuri ni ule na Yesu na mpanzi ( Marko 4:3-8) aliyekwenda kupanda mbegu shambani mwake. Tena kuna hata na wimbo wake. “ Mpanzi alitoka kwenda panda mbegu njema shambani mwake, na nyingine zilianguka kwenye miiba, na nyingne zilianguka pakavu, na nyingine zilianguka kwenye udongo mzurii, zikazaa matunda zikimea na kukua, na kuzaa moja thelathini, moja sitini na moja mia”. Kwa kifupi panda mbegu yako kwenye udongo wenye rutuba, yaani saidia watu wale ambao unajua wanahitaji msaada zaidi kuliko kuwekeza katika miungu mingine.

Maandiko pia yanatuonyesha ya kwamba ni heri kutoa kuliko kupokea (Mdo 20:35). Kwa maana hiyo basi kwa pale unapotoa kwa watu usitegemee kurudishiwa kama ulivyotoa na pengine waweza usirudishiwe kabisa. Jua ya kuwa Mungu ndiyo mpaji, kwa kutoa kwako kwa moyo safi hakika utarudishiwa kwa namna nyingine. Mtolee Mungu kwa moyo wako wote hakika nawe utatimiziwa mahitaji yako. Waebrania 6:14 “Hakika yangu kubariki, nitakubariki na kuongeza nitakuongeza”

Where your treasure is, your heart will be!