Wednesday, April 10, 2013

Neno la leo

Wim 2:11-12 “Maana tazama, kaskazi imepita, Masika imekwisha, imekwenda zake; Maua yatokea katika nchi, wakati wa kupelea umefika, na sauti ya mwigo husikiwa kwetu”

TAFAKARI: Kuna nyakati mtu hupitia misimu ya matatizo mbali mbali na mambo yake yote kuenda mlama. Pengine kwa kila ashikacho hubomoka ama huharibika kabisa. Lakini pindi mlango wa baraka ukifunguka kila kitu huenda sawa.
SALA: Bwana Mungu asante kwa kunionyesha matumaini pale nilipokata tamaa kabisa. Huu ni wakati wangu wa kufurahia matunda yako. Nakushukuru hata kwa mvua na mafuriko yaliyonipata, kwa maana yamenikuza na kunijenga kiakili na hata kuniletea baraka hizi sasa. Asante Mungu kwa upendo wako, Amen.

 

Tuesday, April 9, 2013

Neno la leo

Ebr 1:1-2 “Mungu ambae alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu”

TAFAKARI: Mungu alikuwa na mpango mzuri wa mawasiliano tangu enzi za kale alipowatumia manabii wake. Anajua mambo ya zamani na hata ya baadae yatakayoikumba ulimwengu. Kwa kutambua hilo alimtoa mwanae wa pekee ambae kupitia yeye tutapata kuokolewa.
SALA: Mwenyezi Mungu ulijua ya kwamba watoto wako tunahitaji kusikia sauti yako hata ukapanga mawasiliano mema kati yetu na wewe. Wakati mwingine natamani kama ingekuwa rahisi kuwatambua manabii wako wengine. Lakini kwa kumtoa mwanao Yesu Kristo nimetambua uzuri wako, nimeona na umenijibu maombi yangu. Asante kwa kutoa mawasiliano yaliyo wazi kupitia nguvu za Mwana wako Yesu Kristo, kwa maana kupitia kwake yeye sisi tumepona.

Monday, April 8, 2013

Neno la leo

Mithali 16:9 “Moyo wa mtu huifikiri njia yake; bali BWANA huziongoza hatua zake”

TAFAKARI: Kwa kawaida mioyo yetu inabeba matumaini na mipango yetu ya baadae, lakini mwenye kujua muelekeo wa mipango hiyo ni Mungu pekee. Na mara nyingine tunashindwa kabisa kukamilisha mipango hiyo kwa wakati muafaka hivyo kukata tamaa. Lakini Mungu huwa upande wetu na kutupa nguvu mpya ya kuendelea.
SALA: Asante Mungu kwa kuniwezesha kukaa katika ulinzi wa mipango yako na si ya kwangu pekee. Mara nyingine mambo yanabadilika haraka na ninapoteza mwelekeo, lakini nikipiga hatua ya njia mpya najua unanibeba na kuniinua juu. Asante kwa kuniongoza katika njia nzuri kila siku. Katika jina la Yesu naomba na kushukuru, Amen.

Friday, April 5, 2013

Neno la leo

1Yoh 5:14 “Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia”

TAFAKARI: Mungu husikia kila hitaji la mtu endapo tunamuomba kwa kuamini ya kwamba atatutimizia mahitaji yetu. Masikio yake yako wazi kusikia vilio vya mioyo yetu, hivyo hatuna budi kumuangalia yeye daima.
SALA: Bwana Mungu, asante kwa kunisikiliza. Natambua ya kwamba ni zawadi pekee kwa mimi kujiachia kwako Mungu kwa maana utaniondolea wasi wasi ndani ya moyo wangu. Mara nyingine nimekuwa na maswali ya ajabu na hata kuuliza juu ya mahitaji yangu, lakini wewe hukuacha kunisikiliza. Nakupenda Mungu wangu na kamwe sitaacha kukutumikia wewe. Katika jina Yesu naomba na kushukuru, Amen.

Thursday, April 4, 2013

Neno la leo

Zab 71:5 “Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, Tumaini langu tokea ujana wangu”

TAFAKARI: Ni jambo la faraja sana pale mtu anapompokea Kristo kuwa mwokozi wa maisha yake. Anakuwa mwenye nguvu mpya, mwenye wingi wa busara na hekima na zaidi Imani yake huongezeka maradufu kwa kumtegemea Mungu.
SALA: BWANA, nasema asante kwa nguvu unazonipa kila siku.Yale madirisha madogo ya bahati niliyokuwa nayo sasa yamekuwa milango mikubwa iliyo wazi. Kila kitu kiko sawa nikisimama kwa jina lako. Mungu naomba nizidishie imani hii ili nikadumu kwako daima milele. Katika jina la Yesu naomba na kupokea, Amen.

Wednesday, April 3, 2013

Neno la leo

2The 3:5 “Bwana awaongoze mioyo yenu mkapate pendo la Mungu, na saburi ya Kristo”

TAFAKARI: Ni vizuri kufuata muelekeo mzuri na kuendenda katika zile njia Bwana anatuongoza.Tusichezee mioyo yetu katika kufanya mambo ambayo yanahatarisha na si ya kumpendeza Bwana.Tumuombe Mungu tuzidi kukua katika imani
SALA: Bwana Mungu naomba niwezeshe niendelee kuwa kwenye muelekeo unaotaka niwepo.Nisaidie nisiingie kwenye majaribu ya kuabudu miungu mingine bali wewe. Katika jina la Yesu naomba na kupokea, Amen.

Tuesday, April 2, 2013

Neno la leo

Wakolosai (Kol) 4:6 “Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu”

TAFAKARI: Kuna wakati mtu anakosa maneno yenye busara wakati wa maongezi na wengine. Ama mtu anaweza akose kabisa maneno ya kumwambia mtu aliyefikwa na matatizo kama msiba ama matatizo ya aina yoyote ile. Yatupasa kumuomba Mungu atupe hekima na busara katika kuchagua maneno ya kuongea na wenzetu.

SALA: Bwana Mungu naomba unisaidie niguswe na pendo lako pale ninapotafuta maneno mazuri ya kusemezana na wenzangu. Naomba nipe hekima ya kuweza kutumia kinywa changu kuwabariki wengine nikiongozwa na roho wako mtakatifu. Katika jina la Yesu naomba na kupokea, Amen.